.

Jumamosi, 12 Oktoba 2013

UN WAIMWAGIA SIFA TANZANIA...!!

  Tanzania ikitajwa kuwa ni miongoni mwa nchi zenye amani na utulivu, imebainika kuwa Watanzania ni miongoni mwa watu wasio na furaha na waliokata tamaa hapa duniani.
Ripoti inayoonyesha orodha ya nchi zenye furaha duniani ya mwaka 2013 (World Happiness Report 2013), imeitaja Tanzania kuwa ni miongoni mwa nchi 10 za mwisho duniani kati ya nchi 156 zilizofanyiwa utafiti huo.

Ripoti hiyo iliyoandaliwa na kundi la wataalamu kutoka Umoja wa Mataifa (UN), kati ya mwaka 2010 na 2012, inaonyesha kuwa Tanzania imeshika nafasi ya 151 ikiburuta mkia pamoja na nchi za Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Benin na Togo.
Upatikanaji wa huduma za jamii, mtazamo wa watu kuhusu rushwa, umri wa kuishi, ukosefu wa kazi, pato la taifa na ukarimu wa watu katika nchi husika, ni baadhi ya vigezo vilivyoangaliwa wakati wa kuandaa taarifa hiyo.
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alieleza kushtushwa na ripoti hiyo kwa maelezo kwamba ni asilimia 11.7 tu ya Watanzania wasio na ajira na kwamba wale wanaofanya kazi, wanapata huduma zote za msingi, ikiwa ni pamoja na kwenda likizo na mishahara inayolingana na taaluma zao.
“Watanzania wana furaha, kwa upande wa wafanyakazi wanapata haki zao zote wanazostahili, sijui ni vigezo vipi wametumia…kwa mujibu wa takwimu za 2006 ni asilimia 11.7 ya Watanzania ndio waliokuwa hawana kazi, lakini wakati huo idadi ya watu ilikuwa ndogo, hivi sasa imeongezeka,” alisema Kabaka na kuongeza:“Usafiri ndiyo tatizo linalowasumbua wafanyakazi wengi kwa kuwa wanachelewa kwenda kazini.”
Naye, Naibu Waziri wa Fedha, Saada Salum alisema pamoja na vigezo vingine vilivyotumika kutambua furaha ya Watanzania, umaskini ndiyo unaoweza kuwa chanzo cha Tanzania kushika nafasi za mwisho.
“Inategemea na vigezo vingine walivyovitumia, nakubali kuwa Tanzania ni maskini pengine hali hiyo imeifanya nchi kushika nafasi ya mwisho,” alisema Salum.
Nchi zilizoongoza
Taarifa hiyo imezitaja nchi tano; Denmark, Norway, Uswisi, Netherlands na Sweden kuwa ndizo zinazoongoza kwa watu wake kuwa na furaha zaidi duniani, huku Angola ikishika nafasi ya kwanza Afrika na ya 61 duniani ikifuatiwa na Algeria (73), Libya (78), Ghana (86), Zambia (91), Lesotho (98), Morocco (99) na Swaziland (100).
Kwa upande wa Afrika Mashariki, wananchi wa Uganda ndio walionekana kuwa na furaha zaidi kwani nchi hiyo imeshika nafasi ya 120 wakifuatiwa na Kenya (123), Tanzania (151), Rwanda (152) na Burundi (153).
Ripoti hiyo inabainisha kuwa kati ya mwaka 2005 na 2012, nchi 60 duniani ziliongeza viwango vya furaha kwa watu wake, kati ya hizo 16 zikiwa barani Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Mtete Focus Blog

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni