.

Ijumaa, 27 Desemba 2013

Hatimaye Rasimu kuhusu mahakama ya Kadhi Zanzibar yakamilika....!!


Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema Rasimu ya Mahakama ya Kadhi imekamilika na inatazamiwa kuwasilishwa katika ngazi za makatibu wakuu kabla ya kufikishwa  kwenye Baraza la Mapinduzi.

Waziri wa Sheria na Katiba, Abubakar Khamis Bakary, alisema jana kuwa Rasimu hiyo ambayo inasubiriwa kwa hamu na makundi ya watu wakiwamo wanaharakati baada ya kupata baraka za Baraza la Mapinduzi itawasilishwa kwenye Baraza la Wawakilishi mwakani.

Alisema Rasimu hiyo imeandaliwa kwa ajili ya kuboresha mfumo wa kuendesha Mahakama za Kadhi ili uwe na ufanisi na  kutatua migogoro ikiwamo ya ndoa kwa Waislamu.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mdungi Ussi, alisema Rasimu hiyo ina lengo la kuimarisha na kuweka mfumo mzuri wa kuendesha mahakama za kadhi nchini.

Alisema kwa muda mrefu yapo malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu muundo wa Mahakama ya Kadhi na utaratibu wa kuendesha kesi na kutoa uamuzi: "Rasimu ya Mahakama ya Kadhi kwa kiasi kikubwa itaondoa malalamiko yaliyokuwapo awali ikiwamo wanaume kutelekeza wake na matunzo ya watoto," alisema.

Miongoni mwa mambo ambayo yalijadiliwa kwa kina likiwamo suala la wanawake kupata mgawo wa mali  wanapoachwa na waume zao na suala la matunzo ya watoto, ambapo kwa kawaida mwanamke anapopewa talaka huachiwa malezi ya watoto.

Kwa mujibu wa utafiti lipo wimbi kubwa la talaka na tatizo la wanawake kutelekezwa na waume zao  na watoto.

Katika mkoa wa Kaskazini Unguja mwaka 2012/13 talaka 53 zilitolewa huku wanawake wakitelekezwa na waume zao na watoto kwa mujibu wa karani ya Mahakama ya Kadhi Mkokotoni, Asma Francis.

Aidha, kesi 10 za wanawake kutelekezwa na kudai matunzo ya watoto zilifikishwa katika Mahakama ya Kadhi ili kupata ufumbuzi huku wanaume wawili wakikubali kutoa fedha za matunzo ya watoto.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni