.

Ijumaa, 22 Novemba 2013

UFAFANUZI WA CHADEMA KUHUSU MAAZIMIO YA KAMATI KUU


Live Updates: Ndugu Wanachama na Watanzania na wote muda si mrefu tutawaletea Mkutano na Waandishi wa Habari kuwajulisha Watanzania maazimio na maamuzi ya Kamati Kuu iliyokutana kwa siku mbili tarehe 20-21/11/2013 katika Hotel ya Blue Pearl Ubungo Plaza jijini Dar es Salaam

================
UPDATES

- M/Kiti Mh. Freeman Mbowe ameshawasili na ameanza kwa kusema kuwa Kamati Kuu imemteua Mh. Tundu Lissu kuwa Mwanasheria Mkuu wa Chama na pia Kamati Kuu imefikia maamuzi ya kinidhamu kwa baadhi ya viongozi.

Anamkaribisha Mh. Tundu Lissu kwa ajili ya kutoa taarifa ya maazimio ya Kamati Kuu kwa niaba ya M/Kiti

- Tundu Lissu anaanza kwa kusema kuwa Kamati Kuu imenasa waraka wa mkakati wa siri wa kukipasua Chama vipande vipande unaohusisha watu wanne ambao ni Zitto Kabwe, Dr. Kitila Mkumbo, Samson Mwigamba na mtu mwingine ambaye hajajulikana.

- Anasema lugha iliyotumika katika waraka huo ni ya siri ambapo kuna mtu anaitwa MM ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Zitto Kabwe, M1 ni Dr. Kitila Mkumbo, M2. Hajajulikana na Dr. Mkumbo alikana kumfahamu kabisa M2, na M3 ni Mwigamba.

Lissu anasema Waraka huo uliojulikana kama Waraka wa Ushindi unavunja katiba ya Chama kwa sababu umepandikiza chuki za kidini, majungu na kukashifu viongozi wa Chama kinyume na katiba ya CHADEMA.

Lissu anasema tuhuma zote zilizoko katika waraka huo hazijawahi kuwasilishwa kwenye kikao chochote halali cha chama kinyume na matakwa na masharti ya katiba yetu

- Anasema Kamati Kuu imeamua kuwavua nyadhifa zao zote watu wote waliotajwa katika waraka huo ambao ni Zitto Kabwe, Dr. Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba.

Pia kamati kuu imeunda kamati ya kuchunguza na kufuatilia mhusika mwingine M2 ambaye anadaiwa ni Mtumishi wa Makao Makuu ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa dhidi yake

Kamati Kuu imeagiza wahusika wote waandikiwe barua za kujieleza ni kwanini wasivuliwe uanachama kwa makosa hayo makubwa waliyofanya.

- Pia Kamati Kuu imeagiza mchakato wa kumvua Zitto nafasi yake ya Unaibu wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

- Lissu anasema Naibu Katibu Mkuu Zitto Kabwe na Dr. Kitila Mkumbo waliomba kujiuzulu nyadhifa zao zote baada ya waraka wao kukamatwa lakini Kamati Kuu iliwakatilia baada ya kuona kuwa kukubaliana na maombi yao hayo ilikuwa ni kama kuwaacha wajiuzulu kwa heshima ambayo hawaistahili hata kidogo.

- Kamati Kuu pia imeazimia kuusambaza waraka huo kwenye vyombo mbalimbali vya habari ili watanzania waone na kujua ukweli.

Lissu anamalizia kwa kuwaomba watanzania na Wanachama wote wa CHADEMA nchi nzima wasife moyo na waendelee kukijenga Chama na nchi yao.

- Kamati Kuu pia imemteua Wakili Msomi Mh. Peter Kibatara kuwa Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu wa Chama

- Mh. Mbowe anasema waraka wa siri za Zitto haukutengenezwa wala haukutoka Makao Makuu. Alikuwa akijibu swali la Mayage kuhusu zitakapopatikana fedha za kutekeleza mpango huo

Jamii Forums

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni