.

Jumatano, 5 Novemba 2014

JK: Naomba yasinikute ya Warioba


warioba+px.jpg
warioba+px.jpg (55.98 KiB) Viewed 75 times


Rais Jakaya Kikwete amesema anaomba yasimkute ya Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya


Jaji Joseph Warioba akiokolewa katika vurugu zilizotokea wakati wa mdahalo kuhusu Katiba Dar es Salaam juzi.

Dar/mikoani. Rais Jakaya Kikwete amesema anaomba yasimkute ya Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba aliyeshambuliwa katika mdahalo wa katiba uliofanyika Dar es Salaam, juzi.

Rais Kikwete alitoa kauli hiyo Mwanza jana katika mkutano wa 12 wa Shirikisho la Taasisi za Kupambana na Rushwa (Safac) unaojumuisha nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc).

“Naamini Katiba Inayopendekezwa itapitishwa, nina matumaini hayo. Nadhani na mimi nitakavyokuwa napiga kampeni hayatatokea yale ya jana(juzi), maana mie sioni haya kuipigia kampeni kama wale wenzetu ambao wanataka isipite,” alisema Rais Kikwete kwa ufupi.

Juzi, Jaji Warioba alishambuliwa na kundi dogo la watu walioingia katika mdahalo ulioitishwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere na kutolewa chini ya ulinzi.

Vurugu hizo zilitokea wakati Jaji Warioba alipokuwa akihitimisha hotuba yake kwa kuhoji watu wanaotumia vibaya jina la Mwalimu Julius Nyerere kupitisha hoja zao katika misingi isiyokubalika.

Miongoni mwa wanaotuhumiwa kumshambulia Jaji Warioba ni Katibu wa Hamasa wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana (UVCCM), Paul Makonda ambaye hata hivyo, jana alikana kufanya kitendo hicho.



Tukio lakemewa kila kona

Wasomi, wanasiasa na wananchi wa kada mbalimbali nchini wamelaani vurugu zilizotokea katika mdahalo huo na zaidi, kitendo cha Jaji Warioba kuvamiwa na kupigwa.

Mbali na kulaani, mjumbe wa iliyokuwa Tume hiyo, Profesa Mwesiga Baregu alimtaka Rais Kikwete kutoa tamko, huku wanaharakati na wasomi wakitaka ulinzi uimarishwe kwa viongozi wa kitaifa wakiwamo wastaafu.

Profesa Baregu alisema ni vizuri kwa Rais akatoa tamko kuhusu tukio hilo ili kunusuru mchakato mzima wa Katiba Mpya.

“Nashangaa mpaka sasa Serikali imekaa kimya licha ya kutokea kwa tukio hili la aibu kwa Taifa, ambalo unaweza ukahisi lilipangwa ili kuhatarisha usalama wa wananchi,” alisema na kuongeza:

“Jaji Warioba kwa wadhifa wake, anatakiwa kupatiwa ulinzi wa kutosha kama walivyo viongozi wengine wastaafu, lakini cha kushangaza jana (juzi) mpaka tunaanza mdahalo hakukuwa na askari hata mmoja ndani ya ukumbi, badala yake walikuwa nje ya jengo lile.”

Alisema kwa mwenendo uliopo sasa, itakuwa vigumu kupatikana Katiba Mpya kwani wananchi wanakoseshwa haki zao za msingi ikiwamo usalama.

Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha), Halima Mdee alilaani kitendo hicho na kuitaka Serikali kuwachukulia hatua kali waliohusika.

Akihutubia mkutano wa hadhara katika Kata ya Nyalikungu Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu, Mdee alimtuhumu Makonda na wenzake kuwa wamefanya tukio ambalo limeidhalilisha nchi.

“Tunalaani vikali kilichomtokea Warioba ...nani asiyefahamu uadilifu wa Warioba? Eti wanampiga, hili hatuwezi kukubali litokee tena. Serikali iwachukulie hatua kali kwani waliofanya wanajulikana kwa nini kuwaficha au kosa la Warioba ni lipi?”

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana alisema viongozi wa kitaifa wanatakiwa kupewa ulinzi wa kutosha na kitendo kilichotokea juzi ni aibu kwa Taifa zima.

Mwenyekiti wa PPT - Maendeleo, Peter Mziray alisema viongozi wastaafu wasijihusishe kabisa na masuala ya kisiasa badala yake wapumzike kama alivyoamua Waziri Mkuu mstaafu, Cleopa Msuya.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alikataa kuzungumzia lolote akisema yupo nje ya nchi.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba la Tanzania (Jukata), Deus Kibamba alisema vurugu hizo ni maafa na uhuni wa kutisha unaostahili kulaaniwa.

“Sitaki kuamini kuwa wale vijana wahuni walitumwa na CCM, sitaki kuamini hata kidogo… hali ile ni maafa. Ulinzi na usalama umekwisha kabisa,” alisema na kuongeza: “Hii hali ya kusubiri mpaka maafa yatokee haifai. Warioba ana mlinzi mmoja na sisi jana tulikuwapo pale ilifikia kipindi hadi walinzi wa Jukata waliingia kumsaidia Warioba, ni aibu kubwa.”

Mtafiti wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Patience Mlowe alisema vurugu hizo zimemshangaza kila mpenda amani na demokrasia.

“Ni fedheha kwa Taifa. Warioba ni Makamu wa Rais na Waziri Mkuu mstaafu, halafu vijana wanashindwa kumheshimu… hili ni janga kwa Taifa,” alisema Mlowe.
ADVERTISEMENT

Mbunge wa zamani wa Vunjo, Aloyce Kimaro alisema kitendo alichofanyiwa Jaji Warioba hakijawahi kufanywa tangu nchi ipate uhuru na kwamba waliofanya kitendo hicho wanataka kuharibu utawala wa Rais Kikwete ambaye amewapa Watanzania uhuru wa kuzungumza.

“Hao wahuni waliompiga Warioba walionekana vizuri kwenye runinga. Serikali iwachukulie hatua kali kwa kuwa wamedhalilisha nchi, pia Watanzania tujifunze kusikiliza maoni ya mtu hata kama yanakukera,” alisema.

Mwasisi wa Chadema, Edwin Mtei aliwataka Watanzania kulaani kitendo hicho huku akimtaka Jaji Warioba asikate tamaa, bali aendelee kutetea maoni ya wananchi.

Mtei alisema kilichofanyika ni sawa na laana kwa vijana kwani haiwezekani kuwashambulia wazee wenye heshima kubwa katika Taifa bila sababu za msingi.



CUF kulinda midahalo

Chama cha Wananchi (CUF) mbali ya kulaani, kimekwenda mbali na kikisema kinachukua dhamana ya kuilinda midahalo yote itakayomhusu Jaji Warioba, waliokuwa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko Katiba na Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), kwa nia njema ya kutoa elimu ya uraia juu ya Katiba Inayopendekezwa.

Taarifa ya Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Abdul Kambaya ilisema chama hicho kimeamua kuchukua dhamana hiyo kwa kuwa polisi wameshindwa kutekeleza wajibu wao.

“Jaji Warioba ni kiongozi wa Taifa hili, hivyo kwa namna yoyote ile hawezi kudhalilishwa huku CUF kama wadau wa mambo ya siasa na elimu ya uraia tukiwa kimya,” ilisema taarifa hiyo ya Kambaya.



Makonda ajitetea

Wakati wanasiasa na mitandao ya kijamii ikimlaani Makonda, kiongozi huyo jana aliitisha mkutano wa waandishi wa habari na kusema hakumpiga Jaji Warioba, bali alikuwa akimwokoa katika vurugu hizo.

Makonda alisema baada ya vurugu hizo kutokea, aliamua kumwokoa Mjumbe wa lililokuwa Bunge Maalumu la Katiba, Amon Mpanju na Jaji Warioba ili wasijeruhiwe kwenye vurugu hizo. Picha zilizochapishwa jana zilimwonyesha Makonda akiwa amemshika Jaji Warioba.

“Nilipoingia ukumbini nilikwenda kukaa jirani na Mpanju, baada ya kutokea vurugu nikaona ni lazima nimwokoe kwa sababu ya ulemavu wake wa kutokuona. Jaji Warioba alituona na akanisogelea akaniambia nisimwache Mpanju asije akapata matatizo. Kwa hiyo nikawa niko karibu na Mpanju na Warioba ili kuhakikisha kuwa wanakuwa salama.”

“Warioba ni kama baba yangu, kamwe siwezi kunyanyua mkono wangu na kumpiga, nitakuwa ninajitafutia matatizo, huu ni mchezo mchafu unaochezwa na baadhi ya wanasiasa wenye lengo la kunichafua.

“Leo (jana) asubuhi Warioba amenipigia simu akinipa pole kwa vurugu hizo, nami nikampa pole kwa yote yaliyotokea jana, sasa inakuwaje mtu uliyempiga halafu akakupigia simu ya kukupa pole?” alisema Makonda.

Hata hivyo, Jaji Warioba hakupatikana jana kuzungumzia nini hasa kilitokea kati yake na kada huyo wa CCM ambaye pia alikuwa mjumbe wa Bunge la Katiba.



Kauli ya Polisi

Msemaji wa Polisi, Advera Bulimba alisema bado viongozi wastaafu wanapatiwa ulinzi wa kutosha lakini hakutaka kufafanua zaidi vigezo vinavyoangaliwa kwa kile alichoeleza kuwa ni sababu za kiusalama,” alisema.

Mwaka 2009 Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi alipigwa kibao shavuni alipokuwa akihutubia katika Baraza la Maulid.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema watu kadhaa ambao hata hivyo hakuwataja kwa majina wala idadi, walihojiwa ili kujua chanzo cha vurugu hizo na kuwa uchunguzi unaendelea.
 Sorce tanzania forum

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni