.

Jumamosi, 4 Oktoba 2014

Uzuri wamponza dada huyu


WASICHANA ndugu wanaokadiriwa kuwa na umri wa miaka 16 na 18 wamemshambulia kwa visu binti mwenye miaka 15, kwa lengo la kumkomesha kwa sababu anasifiwa kuwa mzuri. 
 
Katika tukio hilo la aina yake, ndugu hao walimvizia msichana huyo, Julia Alvarez(15), njiani wakati anakwenda nyumbani mjini Juan Domingo Peron kwenye jimbo la Formosa Kaskazini mwa Argentina.
 
Kwa mujibu wa kauli za wasichana hao, walifanya unyama huo kwa kuwa hawakupenda kusikia sifa alizokuwa anapewa binti huyo kuwa ni mrembo sana.
 
Mwathirika huyo, Alvarez alisema wakati anashambuliwa, wasichana hao walisema, walitaka kumharibu awe anatisha kama mcheza sinema za kutisha, Chucky.
 
Msichana huyo alisema alivamiwa wakati anakwenda nyumbani kujiandaa kwenda kuwatembelea rafiki zake, wasichana wawili walimvamia, wakaanza kumpiga na kumwangusha chini. Alvarez amesema, baada ya yeye kuanguka, wasichana hao walitoa visu na wakasema,
 
“Kila mtu anasema una mvuto, tukikumaliza mvuto wote utaisha, watu watakuita Chucky”. Mtoto huyo alikatwa kwa visu kwenye sehemu mbalimbali mwilini hasa usoni na mgongoni. Baada ya kumuumiza binti huyo, wasichana hao walikimbia na kumwacha amelala kwenye dimbwi la damu, mpita njia alimwona, akamkimbiza hospitali.
uzuri
 
Inadaiwa kuwa, awali polisi hawakuchunguza tukio hilo lakini dada wa majeruhi aliweka picha za mdogo wake kwenye mtandao wa facebook, ndipo watu wakashinikiza haki itendeke. Wasichana waliomshambulia Alvarez wakamatwe.
 
“Walimwonea wivu mdogo wangu kwa muda mrefu, na kila mara walimkashifu na kumtukana lakini hatukutarajia kufika mbali kiasi hiki. Nimejaribu kuwa mvumilivu kwa ajili ya mdogo wangu mrembo lakini kila mara nikimwona nataka kutokwa machozi, wameharibu maisha yake,” amesema mwanamke kwenye ukurasa wa facebook akijitambulisha kuwa ni dada wa binti aliyejeruhiwa.
 
“Alisema anataka kujiua kwa sababu sasa akijitazama kwenye kioo anajiona mbaya, imeharibu familia yetu,” alieleza mwanamke huyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni